Monday, November 21, 2022
Maana ya Zip code.... Orodha ya Post code Tanzania
Saturday, November 12, 2022
Wednesday, August 17, 2022
Mbinu 7 rahisi za kufanya ubongo wako kuwa nadhifu (kulingana na Chuo Kikuu cha Harvard)
Mojawapo ya athari za baada ya Covid-19 ilikuwa wazo kwamba ukungu wa ubongo-na athari zake kwa akili zetu na kumbukumbu ya muda mrefu-zilikuwa kweli kabisa. Kila mtu aliyetoka ndani yake alianza kukisia kama bado walikuwa mkali kama walivyokuwa kabla ya virusi kuanza. Na ingawa wengi wetu huenda tusipate jibu la swali hilo linalotia wasiwasi, hakika kuna suluhu kwa hilo. Kulingana na mfululizo wa tafiti na utafiti wa Chuo Kikuu cha H
arvard, si jambo gumu kufanya ili kunoa akili yako kwa mambo rahisi unayoweza kufanya kila siku. Iwe ni kukuza kumbukumbu yako au kutoa changamoto kwa akili yako kufanya mambo kwa njia tofauti, hila hizi zitakusaidia kuboresha uwezo wako wa ubongo kama vile kutokufanya biashara yoyote.
1. Jifunze Mchezo Au Ustadi Mpya

Ifikirie kama kukunja misuli ya akili yako. Kila wakati unapojiweka kwenye jukumu la kupata ujuzi mpya–sema, kujifunza lugha au jinsi ya kupika kitu kilicho tata zaidi kuliko tambi za papo hapo–unasisimua seli za ubongo wako na mawasiliano kati yao. Ikiwa huna muda wa kujifunza Kirusi au Veal consommé, usifadhaike. Hata kufanya mchezo mgumu wa jigsaw puzzle au mchezo wa kumbukumbu kunaweza kufanya akili yako ifanye kazi.
2. Changamoto Hisia Zako
Uchunguzi unaonyesha kuwa kadri unavyojihusisha zaidi na hisi yako katika mchakato wa kujifunza kitu, ndivyo uwezekano wa kuhifadhi kumbukumbu hiyo unavyoongezeka. Katika utafiti mmoja ambao Harvard alifanya, kikundi cha kuzingatia kilionyeshwa anuwai ya picha zisizo na kihemko, ambazo kila moja iliwasilishwa na harufu. Hakuna maagizo yaliyotolewa kuhusu kujaribu kukumbuka kile walichokiona. Baadaye, walionyeshwa mfululizo wa picha, safari hii bila manukato, na kutakiwa kubainisha ni zipi walizoziona hapo awali. Masomo yalikuwa na kumbukumbu bora kwa picha zote zilizooanishwa-hasa zile zinazohusishwa na manukato ya kupendeza. Picha ya ubongo ilionyesha gamba la piriform (eneo kuu la ubongo la kuchakata harufu) lilianza kuwa hai watu walipoona vitu vilivyooanishwa na harufu.
3. Sema Mambo kwa Sauti
Kitendo rahisi cha kusikia maneno kwa sauti huwafanya kuwa na uwezekano mkubwa wa kushikamana nawe–kama vile mchakato wa kuyarudia. Hili hufanya kazi vyema hasa unapojifunza kitu-kama kukutana na mtu mpya. Ukitambulishwa kwa mtu mpya, na ukitumia jina lake mara chache katika mazungumzo ya kwanza uliyofanya naye, kuna uwezekano kwamba utaunganisha sura zao na jina lake na kulikumbuka kwa urahisi zaidi baadaye.
4. Gawanya Habari katika Vipande
Mfano mkuu ni kujaribu kujifunza nambari ya simu (ingawa, kwa simu za rununu, hatujalazimika kufanya hivyo kwa miaka mingi). Huna uwezekano wa kukumbuka nambari ya seli ikiwa unaifikiria kama nambari ya tarakimu kumi. Lakini ivunje vipande vipande; tarakimu 3, tarakimu 3, tarakimu 4, au tarakimu 5 na 5, na kuna uwezekano mkubwa wa kuzikumbuka kwa moyo. Gawanya habari vipande vipande na uichakate dhidi ya kuifanya kwa ujumla na unaweza kujikuta ukihifadhi mengi zaidi.
5. Unganisha Habari za Zamani kwa Habari Mpya
Iwe ni kutumia vifaa vya kumbukumbu ili kuboresha kumbukumbu yako au kuunganisha vipande vya taarifa mpya na mambo ambayo tayari yapo katika maisha yako, hii hufanya kazi kama vizuizi vya kujenga akili na kumbukumbu thabiti. Kadiri taarifa tofauti zinavyofungwa kwa kila mmoja, ndivyo inavyokuwa na nguvu na isiyoweza kuvunjika akilini mwako. Ukijitahidi kuunganisha habari mpya na mambo ambayo tayari yanafaa kwa maisha yako, una nafasi nzuri ya kukumbuka yote mawili.
6. Piga Mswaki kwa Mkono wa Kinyume chake
Kusafisha meno yako ni mfano, lakini kimsingi kujaribu kuwa ambidextrous (ikiwa sio), husukuma ubongo wako kufanya kazi kwa bidii kufanya kazi sawa, na kuifanya iwe kazi zaidi. Unaweza kujaribu kuandika, kula, au hata kutuma ujumbe mfupi kwa mkono wako wa kushoto (ikiwa una mkono wa kulia—au kinyume chake), ili tu kuwa na mazoea ya kutumia zote mbili. Hii inatia changamoto akili yako kufanya miunganisho tofauti na kuzuia (kwa kiwango fulani pekee, bila shaka) kuzorota kwa umri.
7. Sitawisha Maisha ya Kijamii
Si lazima kuwa na hasira hadi saa za asubu
hi mara kwa mara, lakini kuna nyenzo za kutosha kupendekeza kuwa na marafiki ni nzuri kwa akili katika njia nyingi. Kukutana na watu na kujihusisha na mwingiliano wa kijamii kunachukuliwa kuwa mbaya zaidi kuliko maisha ya kutengwa na jamii-ambayo pia yanaweza kuhusishwa na unyogovu. Kukutana na marafiki pia kunamaanisha mazungumzo na mijadala yenye afya, ikijumuisha kujifunza mambo mapya na kuwasiliana na maoni ambayo ni tofauti na yako.
Thursday, May 12, 2022
TAQWA COMPUTER TRAINING CENTRE
Uongozi wa Masjid Taqwa-Vigoa unawatangazia nafasi za masomo ya kompyuta kwa ngazi ya cheti kwa wanafunzi wa daraja la kwanza (level One), yatakayoanza tarehe 16/05/20222.
Kozi zitakazofundishwa ni pamoja ni
- Introduction to Computer
- Microsoft Word
- Microsoft Excel
- Microsoft Publisher
- Microsoft Powrpoint
- Internet and E-mail
- Introduction to electrical a basic( umeme wa majumbani)
- Motor rewinding ( usukaji wa mota aina zote)
- Refrigeration (Ufundi wa friji)
Fomu za kujiunga zinapatikana kituoni Masjid Taqwa au unaweza kuzipata kwa kupakua katika link hapo chini
MAHALI: Kituo kinapatikan Mbagala-Chamazi-mfenesini, vigoa ( Uliza msikiti wa mbegu)
MAWASILIANO: Wasiliana na uongozi kupitia simu namba
- +2555 789 175 058 / +255 654 402 592
Sunday, February 6, 2022
KUSH: DAWA MPYA YA KULEVYA NCHINI SIERRA LEONE
Wakati
janga la madawa ya kulevya kama vile likiendelea katika nchi mbalimbali duniani.
Nchi ya Sierra Leone imegundua dawa mpya ya
haramu inayojulikana kwa jina la Kush ambayo huuzwa kwa bei nafuu, na hivyo
kupendwa na watu wengi nchini humo hususani ya vijana. Na inaripotiwa kuwa dawa
hii huenda ikawa na ukali zaidi ya dawa za kulevya kama vile heroin na cocein.
Ripoti
ya hospitali kutoka mji mkuu wa nchi hiyo Free town inasema kuwa “asilimia
tisini (90%) ya wanaume walilazwa katika hospitali hiyo wamekutwa na ugonjwa wa
akili kutokana na matumizi ya kush.
Jeshi
la polisi katika nchi hiyo imejiandaa vikali juu ya matumizi na usambazaji wa
dawa hizo haramu.
Chanzo:
BBC
Monday, November 1, 2021
Saturday, October 30, 2021
ADILI NA NDUGUZE - sehemu ya 5
ADILI NA NDUGUZE - 5
Simulizi : Adili Na Nduguze
Sehemu Ya Tano (5)
Adili alipelekwa katika hazina ya majini iliyokusanya utajiri wote wa ulimwengu. Johari ndogo katika hazina hiyo ilikuwa na uzito usiochukulika kwa Adili. Alipochaguzwa kuchukua alichopenda hakuweza kuchagua kitu chochote.
Malkia alisikitika akasema, "Haidhuru!" Alishika simu akauliza" Naweza kusema na mfalme wa majini?"
Jibu lilikuja , " Naam, Kisasi huyu! Nani mwenzangu?" " Mjeledi , Malkia wa majini ndiye asemaye. Adili amechaguzwa apendacho katika hazina yetu, lakini ameshindwa kuchukua hata kitu cha uzito wa sindano moja. Wanadamu hawajaweza kutumia uwezo waliopewa kama Majini. Nataka msaada wako."
" Vema. Mlete hapa," kengele iliishilia.
Adili alikwenda katika halmashauri ya Majini. Alipofika mfalme alikuwa amekaa kitini kwa juu kuelekea hadhara kubwa ya mawaziri. Joho la mfalme lilikuwa la rangi ya fua, na kichwani alivaa taji la zari. Mawaziri walivaa majoho meusi, na vichwa vyao vilikuwa wazi. Hadhara nzima ilisimama Adili alipotokeza . Ilipokaa kitako tena alipewa kitabu cha hawala ya hazina ya majini. Kwa kila hawala iliyoandikwa na kutiwa sahihi ilipochomwa Adili aliweza kupata alichotaka katika hazina ya majini. Alifurahi kwa zawadi ile. Ilikuwa nyepesi kuwekeka, rahisi kutumika, nayo si nzito kuchukulika. Alimshukuru mfalme wa majini akarudi kwa Huria.
Adili aliyageukia Manyani akauliza kama yaliyosemwa yalitokea au hayakutokea . Manyani yaliziba nyuso zao kwa viganja vya mikono yao kwa aibu.
Nduguze kuwa Manyani
Baada ya Adili kutoswa, nahodha alishtuka akauliza nini kilichotumbukia baharini kwa kishindo kikubwa. Kusikia vile ndugu zake walianza kujiliza uongo kuwa ndugu yao amepotea. Nahodha alikwenda kutazama akaona Adili hayuko. Aliamuru kutua tanga na kuteremsha mashua. Lakini sasa dhoruba kali ilianza, na chombi kilichokuwa katika mrama mkubwa, kwa mawimbi makubwa ya upepo na umande, kilipakia maji, omo na tezi, na kulia ja kushoto. Giza kuu lilinyemelea roho za mabaharia. Palikuwa hapatiliki nanga. Kwa hivi tamaa ya kumuokoa Adili ilikatika.
Nahodha alipotaka kujua Adili alivyopotea, ndugu zake walimwambia kuwa ndugu yao aliamka akaenda msalani. Ghafula walisikia anguko kubwa majini. Watu wote jahazini walisikitika kupotelewa na Adili. Ndugu zake walilizana kitambo wakanyamaza. Kilio cha kujisingizia hakina machozi wala matanga.
Hasidi na Mwivu walichukua sanduku la Adili wakalifungua. Walitoa majohari yote wakagawana mafungu mawili usiku ule ule. Sasa ugomvi kati yao ulianza juu ya yule msichana mzuri aliyekuwa chomboni. Hasidi alitaka kumwoa, na Mwivu kadhalika alitaka kumwoa. Asiyefurahia heri ya mwenziwe, shari yake kumghadhibikia. Walimsahau ndugu yao aliyepotea dakika chache zilizopita kama aliyekufa miaka kumi iliyopita. Walikuwa na mioyo migumu iliyoje!
Mwelekevu, yule msichana mzuri, alikuwa hana tabasamu. Uzuri wake ulisawazika kwa machozi ya njia mbili usoni. Huzuni ilimshika vibaya, lakini alikuwa imara kutetea heshima yake. Aliwaambia wale ndugu wawili wasigombane bure. Hakuwa tayari kuolewa na yeyote kati yao. Na kabla ya sauti ya maneno aliyosema haijaishilia masikioni mwao, alijitosa baharini akatoweka vile vile.
Hasidi na Mwivu hawakujua la kutenda. Atakaye makaa ya mgomba hapati kitu ila jivu tupu. Ndugu hawa wawili walimtosa ndugu yao kwa tamaa ya kupata msichana , lakini walipata aibu tupu. Walikaa kitako wamefedheheka, walipokuwa katika hali hiyo na jahazi inakwenda mbio, Huria na Adili walitua ghafula kama ndege chomboni.
Marejeo ya Adili yalishangaza watu chomboni. Macho ya ndugu zake yalisutana. Kwa kutahamaki walimkumbatia wakajifanya kumfariji. Walisema hatari yake ilitisha, na msiba wao ulikuwa mkubwa. Watu wengine wote chomboni waligeuza macho yap kando waliposikia uongo wa ndugu zake. Walakini Adili aliwashukuru akisema bahari haiweki amana ya kitu kieleacho, kwa kuwa alielea aliokoka.
Kwa hasira kubwa Huria alinena, "kama mngalijua hatari ya kumtosa mtu baharini, au mngalikuwa na fikira za msiba, msingalijaribu kumtumbukiza ndugu yenu baharini alipolala. Wauaji ninyi hamstahili kuishi," aliwashika shingoni pamoja na mkono wa kushoto akawabana kwa nguvu ya ajabu. Mkono wake wa kulia uliinua ngumi juu tayari kuwaangukia kwa uzito mwingi. Ndimi vinywani na mboni machoni mwao zilitoka kwa hofu wakataka kuombewa.
Damu nzito kuliko maji. Hasidi na Mwivu walikuwa damu kwa Adili . Hakuvumilia kuona hilaki yao akamwomba Huria kuwasamehe. Walimtosa tu, hawakumwua. Huria alibisha kuwa walistahili kifo. Jaribu la jinai lilitosha kuhalalisha adhabu ha kifo ujinini. Adili alitaradhia kuwa jaribu la jinai halikutosha kuhalalisha kifo duniani. Kama walikufa kwa sababu yake angalikuwa mnyama wa mwitu mbele ya macho ya watu. Huria aliposikia maneno hayo alinena sheria ya wanadamu ilitatiza. Kwa sababu hiyo walikuwa hatarini milele. Walakini alikubali kuwasamehe kwa sharti ya kuwageuza wanyama. Aliwalaani watoke katika umbo la uanadamu. Mara ile ndugu zake walikuwa manyani.
Kisha Huria aliwakabili watu waliokuwa chomboni akasema. Adili alikuwa rafiki yake mkubwa. Alimjali na kumheshimu juu ya marafiki zake wote. Alipata upendo wake kwa sababu alikuwa salihi na mstahiki wa kuajabiwa na dunia nzima. Ataonana naye mara kwa mara. Mtu yeyote akifitini ataona nguvu ya mkono na uwezo wa ulimi wake. Atampatiliza kama alivyofanya kwa waovu wale wawili. Wajihadhari wapatw kujiokoa kwa sababu alikusdia kutimiza alivyosema. Aliwaonya pia watakapofika kwao wasisemw habari ile. Mtu yeyote atakayejaribu kunong'ona habari ile atakoma kusema milele.
Aliagana na Adili akasema, "Funga manyani haya kwa kamba . Ukifika Jannibu utayafunga kwa minyororo viunoni mbalimbali. Utayatia chumbani na kila moja lifungwe peke yake. Kila usiku wa manane utachukua kiboko ukafungue kila nyani ulipige mpaka lizimie. Utayapa posho na kuyaadhibu hivi daima. Kama amri hii haikutiiwa utaadhibiwa wewe." Alipokuwa akitoa amri hii alijibadilisha sura za ajabu kila dakika moja. Watu wote jahazini walishikwa na mshangao mkubwa kwa mabadiliko yake ya mfululizo, wakatosheka kuwa aliweza kubadili kitu chochote katika umbo alilotaka.
Adili aliyageukia manyani akauliza kama yaliyosemwa yalitokea au hayakutokea. Manyani yaliziba nyuso kwa viganja vya mikono yao kwa aibu.
Adhabu ya Kwanza.
Baada ya kutoweka kwa Huria. Adili alikwenda ngamani kumtazama Mwerekevu. Hakiona mtu. Alipouliza aliambiwa alijitosa baharini ndugu zake walipomkalifu kumuoa. Adili hakuweza kujizuia, akaanguka chini kwa huzuni. Moyo wake ulifumwa kwa msiba akalia kama mtoto mdogo.
Uzuri aliotetea kwa thamani ya maisha yake ulipotea. Aliona wokovu wake haukumfaidia. Bahati ilikuwa mbaya na katili sana kwake. Alifikiri kwamba yeye peke yake ndiye aliyepatwa na ajali mbaya kama ile tangu kuumbwa kwa dunia. Adili aliwaza hivyo, haijulikani mtu mwingine angewazaje.
Kulipokucha chombo chao kilitia nanga Janibu. Matajiri walipanda chomboni wakaamkiana na Adili. Walizungumza mambo mengi, lakini hapakuwa na mtu hata mmoja aliyeuliza habari za ndugu zake. Hili lilimshangaza akamaizi kuwa walio aili walikuwa hawana nafasi katika kumbukumbu za dunia.
Alishuka pamoja na manyani yake akaenda zake nyumbani kwake. Baada ya kuyaweka chumbani alijishughulisha na kupakuwa mali yake. Hakuwahi kutafuta minyororo ya manyani siku ile, na usiku alisahau kuyapiga akalala. Saa saba usiku Huria alitokea na hasira imemjaa tele. Alisema kuwa alikuwa jini. Neno la jini halirudi. Kwa kukosa kutii amri yake adhabu ya kwanza ilimpasa Adili.
Kabla Adili hajajibu neno, mikono yake miwili ilikuwa katika mkono wa kushoto wa Huria. Hakuweza kuponyoka. Kwa mkono wa kulia Huria alimpiga Adili kibao mpaka akazimia. Ndipo alipokwenda yalipokuwa manyani akiyapiga kiboko vile vile mpaka yakakaribia kufa.
Alimrudia Adili aliyekuwa anaanza kupata fahamu akasema, “Twaa kiboko hiki, utayapiga manyani haya kesho usiku kama nilivyofanya. Siku moja ikipita bila kuyapiga, kiboko hiki kitaishia mwilini mwako.” Macheche ya moto yaliyoka kinywani mwake alipokuwa akiamuru hili, na mara neno la mwisho lilipotamkwa alitoweka.
Siku iliyofuata Adili alikwenda kwa sonara akatengeneza minyororo miwili ya dhahabu. Aliileta nyumbani mwaka akaifunga viunoni mwa manyani yake. Usiku alipokwenda kuyapiga na kuyaposha machozi yalimlengalenga machoni.
Katika ini alifumwa na mshale, na moyoni mwake michomo ya maumivu makali. Hakupendelea kuadhibu wanyama waliokuwa kwanza ndugu zake. Huruma yake ilikuwa lakini ilikalifiwa na amri.
Huria alijua huruma ya Adili na kuwa alimkalifu sana. Lakini ndugu zake walikuwa waovu, katili, hiani na wauwaji wa kutisha. Walikosa fikra wakawa duni Kama wanyama wa porini. Adhabu kali kwa waovu ilikuwa ndiyo ulinzi peke yake ya wema. Jini ililiona hivyo, haijulikani mtu angalionaje.
Siku nyingi zilipita, Adili alidhani labda adhabu ya Huria ilikwisha. Siku moja hakuyapiga manyani yake. Loh salale! Dhahama gani? Alijuta kuzaliwa akatamani ardhi ipasuke ajitie ndani yake. Alipigwa kiboko siku hiyo kuliko siku ya kwanza. Mwili wote ulienea makato ya kiboko akavuja damu mpaka akazirai.
Aliteremsha mavazi aliyovaa mpaka kiunoni akaonesha makovu ya mapigo ya Huria. Wepesi wa maumbile wa kuondoa alama haukuweza kufuta makovu ya Adili. Yalijionyesha wazi wazi mwilini mwake.
Toka siku ile na baadaye, hakusahau maumivu ya mapigo yale. Kwa muda wa miaka kumi hapakupita tena hata siku moja aliyoacha kuyapiga manyani yake. Kwa huruma yake kila baada ya kuyapiga aliyanasihi akilia:-
“Nala sumu ndugu zangu
msambe naona tamu,
Takalifu kubwa kwangu,
Kuadhibu yangu damu,
Sina raha ndugu zangu,
Neno hili kwangu gumu.”
Mwisho wa ushahidi, Adili aliyageukia manyani akauliza kama yaliyosemwa yalitokea au hayakutokea.
Manyani yalijiziba nyuso kwa viganja vya mikono yao kwa aibu.
HARUSI
Adili alipolala mtingisho mkubwa ulitokea chumbani mwake sakafu ikapasuka. Kuzinduka uso wake ulikutana na uso wa Huria. Wa kwanza ulijaa matumaini, wa pili ulituna kwa hasira. Nyuso zao zilisomana. Kila uso ulijaribu kuzua mzungu wake.
Adili alivunja amri aliyopewa mara tatu. Alionekana alizoea kuhalifu. Kukomeshwa mazoea yake alipasa kugeuzwa nyani kama ndugu zake. Walakini, kabla ya hili kuwa Huria alitaka kusikia kama Adili alikuwa na udhuru wa kujitetea.
Adili hakusema, lakini tabasamu ya mvuto mwingi ilikuwa ikicheza usoni mwake. Alichukua barua ya Rai akampa Huria. Huria aliposoma barua hakuweza kufanya alilokusudia. Alitoweka akaenda ujinini kumshauri baba yake.
Barua ya Rai ilipowekwa mbele ya Kisasi, kuopolewa kwa ndugu zake Adili kuliridhiwa. Huria alimwuliza Mfalme wa majini labda haja ya Mfalme wa wanadamu isingakubaliwa ingalikuwaje. Baba alieleza.
Mfalme wa wanadamu aliweza kufanya dhara aliyotaka kwa majini. Alikuwa mwanadamu. Mwanadamu alikuwa bora kuliko jini. Majini katika Jua, Mwezi, Mushtara, Zebaki, Zuhura, Mirihi, Sumbla, Zohali, Sarateni, Kausi na Utaridi hayakuweza kushindana na watu katika ardhi.
Majini yaliweza kugeuza watu watu katika umbo lolote, lakini watu waliweza kufunga majini yote katika chupa moja. Magereza yao yalikuwa mabaya sana. Kama mtu asingalikuwa mzembe mwenyewe, busara ya jini ingalikuwa busara yake. Alipasa kuheshimiwa kama alitaradhia heshima yake.
Mara ile Huria alirudi kwa Adili akatangaza kuwa haja ya Rai ilifaulu. Mfalme wa majini alikubali ndugu zake kuwa watu tena.
Aliyabadili manyani akasema, “Tokeni katika uhayawani mrudi katika utu.” Walikuwa watu tena, wakajiangusha miguuni mwa ndugu yao kuomba radhi. Adili alimshukuru Huria, na punde wakaagana.
Asubuhi watumishi walimwona bwana wao na watu wawili. Waliwatambua kuwa walikuwa ndugu zake. Walipouliza kuwa walikuwa wapi kwa muda mrefu, bwana alijibu kuwa walikuwa manyani yaliyoonekana jana yakila naye. Walifurahi kumuona bwana wao si mkichaa, wakamwombea azidishiwe furaha katika maisha yake.
Baada ya kustaftahi aliwavika ndugu zake nguo ali ali, akapanda nao farasi kwenda Ughaibuni. Liwali Adili alipofika Ughaibu na habari kuwa manyani yake yalikuwa watu tena palikuwa na furaha kubwa sana. Jitihadi na kufaulu kwa Rai kuliandikwa katika kumbukumbu za dunia. Hasidi na Mvivu walipoletwa barazani kila mtu aliajabia sura zao. Walikuwa wazuri ajabu.
Mfalme wa Ughaibu alimsifu Adili kuwa alikuwa sababu kubwa ya wokovu kwa ndugu zake katika dhima ya wanyama.
Mateso yaliyompata yalishinda uvumilivu wa mtu. Alivumilia mateso mengi kwa ajili yao. Alikuwa mwanamume barabara na fahari ya Ughaibu. Nchi yake ilimsifu hivi, haijulikani nchi yangu au yako ingalimsifiaje mtu wa namna ile.
Alipogeuka kwa ndugu zake Adili, Rai alionya kama wavivu wajitahidi kuwa hodari, ilikuwa kinyume hodari kuwa mvivu. Kama waovu walitaka kuwa wema, ilichukiza wema kuwa waovu. Kama masikini walitafuta utajiri, ilikuwa ujinga matajiri kufuja walichokuwa nacho. Kama mbegu kidogo iliongezwa mchanga, ilikuwa uharabu mtu kuua ndugu yake. Pia ilikuwa aibu kubwa sana kwa wazuri kutenda maovu.
Wakamilifu walikuwa na nafasi kubwa duniani kuliko wapungufu. Maonyo ya Mfalme yalikuwa mwanana, lakini yalishinda mioyo ya watu waliokusudiwa kuonywa.
Walimshukuru wakaahidi kuwa walikoma kutenda dhara kwa ndugu yao, na kwa kitu chochote kilichokuwa na maisha. Ahadi hii haikuvunjwa.
Mawe huwa dhahabu,
au johari na chuma.
Na mtu anapotubu,
dhambi yake kukoma.
Nidhani zake thawabu,
na heshima ya daima.
Adili alipanda farasi akarudi Janibu na ndugu zake. Njiani alikutana na mabibi watatu waliopanda farasi vile vile.
Mabibi wenyewe walikuwa wazuri na watanashati sana. Wa kwanza alikuwa Mwelekevu aliyeokolewa na Mrefu. Macho ya Adili na ya Mwelekevu yalipokutana mioyo ya giza ilijaa nuru tena. Wote wawili walishuka chini wakaamkiana.
Aha, ilikuwa furaha kubwa iliyoje! Mioyo miwili ya mapenzi iliyopoteana ilikutana tena. Neno halikuwezekana kusemeka. Walitazamana wakachekana. Walishikana mikono wakabusiana. Walikuwa katika siku bora ya maisha yao.
Adili alipomwambia Mwelekevu kuwa wavulana wawili watanashati aliokuwa nao walikuwa ndugu zake, Mwelekevu kadhalika alisema kuwa wasichana wawili warembo aliofuatana nao walikuwa marafiki zake.
Watu wote wanne walishuka chini wakaamkiana vile vile. Kisha wote walipanda farasi wao wakashika njia kuelekea Janibu.
Walipofika palifanywa harusi tatu siku moja. Siku hiyo ilikuwa kubwa kuliko yoyote iliyopita Janibu.
TAMATI
ADILI NA NDUGUZE -sehemu ya 4
ADILI NA NDUGUZE - 4
Simulizi : Adili Na Nduguze
Sehemu Ya Nne (4)
Ulimwengu uliajabia dola yao kwa ushujaa wa askari na kwa busara ya mawaziri wao. Walakini, juu ya sifa hizo, mfalme, malkia na raia walikuwa waabudu mizimu. Mizimu yao ilikuwa miti. Miti yenyewe ni ile iliyogeuka mawe ukutani. Kabwere, Mganga na imamu wa mizimu hiyo alivuta mioyo ya watu wote. Siku moja asubuhi mfalme na malkia walikwenda katika halmashauri zao, kila mmoja akakaa juu ya kiti chake. Madiwani walikuwa wamewazunguka kabla ya kuanza kazi zao za desturi; mtu mmoja ambaye hakujulikana alikotoka alisimama ghafula mbele ya mfalme akajitangaza kuwa aliitwa Mrefu.
Mrefu alikuwa mwujiza katika viumbe. Alikuwa na miguu mikubwa na mapaja manene, kiuno cha utambo na kifua kipana na shingo yake ndefu ilichukua kichwa kikubwa. Mabega yake ya mraba yalining'iniza chini mikono iliyokuwa na nguvu kama manjanika. Kwa kimo cha kukithiri alitembea baharini bila ya kuguswa na maji magotini, akafikia vilele vya milima kwa mikono yake. Aliweza kukamata ndovu chini au nyangumi baharini akamwoka kwa jua mbinguni. Sauti yake ilikuwa kama radi kwa wepesi wake wa ajabu wa kuzunguka dunia nzima kwa sekunde moja, alionekana kama kiumbe kilichoumbwa maalum kuokoa kitu motoni, baharini au katika hatari nyingine.
Mrefu alimwambia Tukufu kuwa mfalme ni naibu wa Mungu duniani. Kwa hiyo , ufalme ni amana kubwa. Amna hiyo ilitaka uangalifu mkubwa kwa sababu ni dhima bora iliyowekwa mikononi mwa wanadamu. Wajibu wa kwanza wa mfalme ni kuwa mwadilifu katika matendo yake. Kila tendo, jema au baya , ni mfano kwa raia wake. Kwa sababu ya maisha ya milele ibada ya mizimu ilikuwa maangamizi , na uimamu wa kabwere ujinga mtupu.
Tukufu alimtazama msemaji akasema kwa ukali, "Nini kilichokujusurisha kusema upuuzi, Mrefu? Kama kwa sababu ya urefu ubongo wako umeyeyuka kwa jua, kaa kitako chini ya kivuli cha mizimu yetu utaburudika. Kama umerogwa, Kabwere atawakomesha waliokuroga. Riziki ya wanadamu hutoka mimeani. Kwa sababu hiyo, mimi na kaumu hii twaabudu miti. Funga ulimi wako, bwana. Usipofunga hasira ya mizimu itakuwa juu yako. Tafadhari jiokoe."
Mrefu alionya , "Hapana haja ya jibu la haraka. Tumia wakati upendao wa kufikiri. Nimesema neno la Mungu. Mungu hachelei tisho la mwanadamu, kazi ya mikono yake mwenyewe. Neno takatifu gumu kufahamika, lakini lina tija kwa wajisumbuao kulifasiri. Kila msaada nitakupa wa kulifasiri."
Tukufu hakujali onyo hili akaamrisha kushikwa kwa Mrefu aliyekuwa hasogeleki wala hashikiki. Uwezo usio hadhari ni kileo kibaya sana. Siku ile ilikuwa ya tisho na msiba, ole na maangamizi makubwa. Kwa laana iliyotamkwa na Mrefu, miji mingine yotw ya dola hii iligharika, na kila kiumbe kilichokuwa na maisha katika Fahari kiligeuka jiwe.
Hili lilipotokea Mwelekevu alikuwa darini anachungulia nje kwa dirishani. Toka pale aliweza kumwona Mrefu na kusikia maneno yake. Hakupendelea kushindwa kwa baba yake. Hapana mtoto apendeleaye hili . Walakini, mapendeleo yakiachwa mbali, nuru ya fikira humulika mno siku zote juu ya kweli kuliko uongo, na juu ya haki kuliko dhuluma. Nuru hii ndiyo iliyomwokoa Mwelekevu katika maangamizi yale ya kutisha. Na tangu siku ile aliamini kuwa onyo la bure likikataliwa huleta majuto ya milele.
Hayo yalipokwisha jiri Mrefu alimpa binti mfalme chuo kitakatifu alichomsifia kuwa bora kuliko vitabu vyote vya duniani vikichanganywa pamoja. Kwa matumizi mengine, Mrefu aliomba mkomamanga uote. Mkomamanga huo ulizaa komamanga moja kila siku. Kila chembe katika komamanga hilo ilikuwa chakula na kinywaji mbalimbali. Kwa mti ule wa ajabu binti mfalme aliweza kuishi maisha ya faraja. Mwisho alionywa kuwa siku ya kuona mti ule umezaa matunda mawili ajue Adili, mwokozi wake amefika. Hilo ndilo lililomjulisha siku ile kuwa mgeni wake alikuwa si mtu mwingine ila Adili.
Usemi wa binti mfalme ulimwonyesha Adili kuwa turufu huenda kwa mchezaji siku zote. Laiti asingalikwenda wenziwe walikoogopa akatafuta tafuta asingalikutana na bahati ambayo hakutazamia kuja katika ndoto zake . Alishukuru akamchukua binti mfalme pamoja na tunu bora alizoweza . Katika tunu zake yalikuwemo pia makomamanga mawili ya ajabu. Hayo yalikomesha kiu na njaa katika merikebu yao kwa muda wa siku kadha wa kadha.
Adili aliyageukia manyani akayauliza kama yaliyosemwa yalitokea au hayakutokea. Manyani yaliziba nyuso zao kwa viganja vya mikono yao kwa aibu.
Kutoswa kwa Adili
Nahodha na mabaharia walimshangilia Adili kama mtu wa bahati ya peke yake, na kuwa mtu mwingine yeyote kati yao angalifuatana naye kwenda walikoogopa , asingalikutana na bahati ile kubwa. Adili aliwashukuru wote akisema kwa furaha mkulima alikuwa mmoja siku zote, lakini walaji wengi. Pato lake lilikuwa pato lao vile vile.
Aligawa tunu zake katika mafungu manne yaliyokuwa sawasaw. Fungu la kwanza alimpa nahodha, na kila ndugu yake akapata fungu moja. Fungu lililobaki lilikuwa lake mwenyewe. Hili aliligawa tena katika mafungu mengi, kila baharia akapata sehemu yake. Isipokuwa ndugu zake, watu wote chomboni walishukuru wakamwombea heri. Nyuso za ndugu zake zilionekana zimekunjamana na macho yao yaliiva. Alifahamu hawakuridhika kwa sababu ya choyo chap kikubwa.
Aliwataka radhi akawaambia kuwa ingawa mafungu yao yalikuwa madogo, lakini wao walikuwa ndugu zake. Mali yake ilikuwa mali yao katika maisha na mauti. Palikuwa hapana sababu ya kukasirika.
Wakati alipokuwa akisema na ndugu zake stahani, Mwelekevu alikuwa amekaa ngamani na jahazi inakwenda moto mmoja.
Sasa Hasidi na Mwivu walimwuliza Adili nia aliyokuwa nayo juu ya bibi yule mzuri aliyempata katika mji wa Mawe.
Aliwajibu kuwa wakifika salama janibu nia yake ilikuwa kumwoa.
Hasidi aliomba kuwa angalifurahi kama angalimwoa yeye bibi yule.
Mwivu kadhalika alinasihi kuwa angalipenda kumwoa yeye.
Kwa kusikitika, lakini kwa imara kabisa, Adili alijibu kuwa kama walitaka neno jingine lolote katika miliki yake angaliwapa, ila hakufikiri kuacha mkono wa bibi yule kuguswa na mru mwingine katika ndoa ila yeye mwenyewe. Wao walimtaka lakini yeye alimpenda zaidi. Walakini wakirudi Janibu atawatafutia mabibi wawili wazuri. Gharama yote itakuwa juu yake. Arusi zao na yake zitakuwa siku moja , fungate na furaha yao itakuwa moja.
Ndugu zake walihoji kama mume mmoja katika Afrika aliweza kuoa wake wengi, na mke mmoja katika Asia alipata kuolewa na waume kadhaa, isingalikuwa vema kama ndugu watatu wa Janibu wangalishiriki uzuri wa mke mmoja?
Adili alibisha kuwa kulikuwa na mambo yaliyofaa na yaliyokuwa hayafai kushiriki. Ndoa ilikuwa jambo moja katika yale yaliyokataa ushirika. Ushirika katika ndoa ulipasa wanyama na ndege. Mtu alitukuzwa mno kuliko mnyama. Huchukiza akiishi katika maisha duni. Ilipasa watu wa wakati ujao katika Afrika, Asia na Janibu kuishi katika maisha bora ya utu, na kuifanya dunia mahali pa kiasi, sio ulafi na uchafu. Mwanamume hakukusudiwa kuwa fahali wa kila mtamba, wala mwanamke kuwa tembe la kila jogoo.
Ushirika wa ndoa ulipofanikisha na uvundo wa kuchukiza duniani, ndugu zake walinyamaza kimya kama walioridhika, lakini moto ulikuwa ukiwaka mioyoni mwao. Usiku Adili alipokuwa amelala na jahazi inakwenda mbio kwa pepo za omo, ndugu zake walikuwa macho. Mawazo mabaya hurusha usingizi. Kuzinduka kwake usingizini Adili alijiona amechukuliwa hangahanga. Kufumbua macho aliona ndugu zake wamemfunga kifati. Mmoja alimshika kichwani na mwingine miguuni. Koo yake ilisongwa sana. Aliwauliza kwa pumzi nyembamba aliyoweza kuvuta neno walilotaka kumtendea.
Alijibiwa , "Huss, fedhuli wee! Wauliza neno ulijualo. Koma sasa! Tumesalitika na mapenzi ya mwanamke aliyeko chomboni. Tumekushauri kumwoa shirika. Umekataa. Huna budi kufa."
Alitoswa baharini kama kitu kilichokuwa hakifai.
Adili aliyageukia manyani akauliza kama yaliyosemwa yalitokea au hayakutokea. Manyani yaliziba nyuso kwa viganja vya mikono yao kwa aibu.
Wokovu wa Adili
Adili alipotupwa alizama kama jiwe katika kilindi cha bahari ambacho urefu wake haukutambulikana. Viwambo vya masikio yake vililia akadhani maji yalipenya sikio hata sikio, na mianzi ya pua yake ilijaa maji yaliyozuia pumzi. Macho yake yalipofumbuka vimemeta kama nyota mbinguni vilionekana katika maji, vimemeta hivyo vilifanywa na mtikiso wa mwili wake. Kutumbukia baharini usiku wa giza ni hatari ya kutisha sana.
Kasi ya kutupwa ilipokoma alijitatamua akakata vifungo vya kamba iliyotatizwa mwilini mwake. Sasa mikono na miguu yake ilianza kufanya kazi. Nusu ya nguvu yake ilikuwa imetumika, lakini matumaini yake yalikuwa kamili. Adili alikuwa si mkata tamaa, na kabla pumzi yake haijakwisha alikusudia kuebuka. Jaribu lake lilikutana na fanaka, maana kabla moyo wale haujakoma alijiona anaelea juu ya bahari. Aliinua kichwa juu ya maji akahema kwa nguvu kama gari moshi. Kulipopambazuka alikuwa katika bahari iliyoghadhibika kwa dhoruba kali, na halibyake ilikuwa taabani. Kutazama hatari usoni kunavunja moyo wa mtu lakini alijikaza kiume.
Mara ile palikuja ndege aliyekuwa na umbo la kutisha akamwopoa Adili majini. Kama koleo, miguu ya ndege ilimshika kwapani akaruka naye. Fikiri wewe mwenyewe hofu aliyokuwa nayo Adili. Binafsi yake alijiona ameokoka kuliwa na papa akawa chakula cha tai. Ndege mwenyewe alipaa juu mpaka Adili alipotelewa na fahamu. Fahamu yake ilipomrudia alijiona katika nyumba kubwa sana iliyokuwa nzuri ajabu. Wasichana warembo na walio changamka walikuwa watumishi katika nyumba hiyo . Miongoni mwao palikuwa na bibi mmoja aliyejipambanua kama malkia, huyo alikaa juu ya kiti cha enzi kilichopambwa na majohari mbalimbali. Rangi ya mavazi yake ilikuwa fua, na kichwani alivaa taji lililopigisha moyo mshindo kwa uzuri.Yule ndege alikuwapo, lakini mara ile alijigeuza msichana wa utanashati mkubwa. Msichana mwenyewe alikuwa yule aliyezama ardhini, baada ya kuokolewa na Adili, alipokuwa katika umbo la tandu na kushambuliwa na nyoka jabalini.
Malkia alimwuliza msichana mtu aliyemwokoa baharini alikuwa nani, na kwa nini aliletwa mbele yake.
Msichana alieleza kuwa mtu yule alikuwa mfadhili wake mkubwa. Zamani maisha yake yalipokuwa katika hatari ya nyoka alipata wokovu kwake. Alimwokoa na kumleta mbele yake kwa sababu aliahidi kulipa fadhili yake.
Kusikia vile, Malkia alisimama akampa mkono Adili aliyeupokea huku amepiga magoti chini. Malkia alimwinua akamkaribisha kuketi kitini akisema, "Starehe, mwanangu. Hali yako ni hali yetu".
Kisha msichana alimwuliza Adili kama aliweza kumtambua yeye alikuwa nani. Adili alijibu kuwa hakuweza.
Msichana alieleza kuwa yeye alikuwa tandu katika jabali fulani zamani akakaribia kuuwawa na nyoka, lakini aliokolewa.
Adili alikubali kuwa alikumbuka kuona tandu jeupe, nyoka mweusi, na msichana aliyezama ardhini.
Tandu lilikuwa yule msichana. Naye alikuwa Huria binti Kisasi. Kisasi alikuwa mfalme wa Majini. Aliyekaa kitini alikuwa mama yake. Jina lake lilikuwa Mjeledi, Malkia wa Majini. Nyoka aliyepigana naye Huria alikuwa waziri wa Ngazi. Alijulikana kwa jina la Hunde. Hunde alikuwa kiumbe cha mwisho katika wanaume waliokuwa na sura mbaya. Siju moja katika matembezi Huria alikutana na Hunde. Alikuwa hatazamiki kwa ubaya, licha ya yeye kumtazama mtu. Pale pale Hunde aliingiwa na shauku kubwa juu ya Huria. Wanawake hukutana na mikasa mingi mibaya duniani. Mioyo yao hulemewa na haja zisizokubalika; masikio yao hutiwa uziwi kwa maombi ya haraka; na miili yao ni mawindo ya jeuri daima.
Hunde alikwenda kwa Kisasi kumposa Huria. Kisasi alijibu Hunde alikuwa ni sufu kwa binti yake ijapokuwa alikuwa waziri wa Ngazi, na kwamba asingalithubutu mbele yake haja kama ile. Tangu siku ile alikomeshwa tamaa ya kuposa mabinti wafalme. Aliudhika akatisha kumwonyesha Huria uwezo wake. Na tangu alipotisha hivyo hakumpa nafasi hata ya uzi kupenya tundu la sindano.
Kila mahali Huria alipopita , Hunde alifuata nyayo zake mpaka aligundua alikokuwa. Iliendelea hivyo mpaka Kisasi akapigana naye. Alishindwa akakimbia. Huria alipotaka kutembea alijigeuza umbo la mnyama. Kila alipojigeuza na yeye alijigeuza vile vile akanusa harufu yake kama mbwa. Alipojigeuza panya, yeye alikuwa paka, alipojifanya paka, yeye alijigeuza chui; na alipokuwa chui, yeye akawa simba. Kila alipoingia yeye alipajua kwa kufuata nyayo zake. Wanaume wana inda mbaya ufisadi unapowapofusha.
Siku aliyojigeuza tandu , yeye alikuwa nyoka akamfukuza. Alipochoka kukimbia alimkamata. Kabla hajamhasiri, Adili alimpiga jiwe akafa. Alijigeuza mtu akaonekana na Adili kwa macho yake. Kabla ya kujizamisha chini aliahidi kulipa wema kwa Adili.
Huria aliomba dua siku zoye ya kuweza kutimiza ahadi yake kwa Adili. Siku aliyotoswa baharini na ndugu zake alikuja upesi kumwokoa katika hatari. Ilipasa wazazi wake, Mfalme na Malkia wa Majini kumkirimu mfadhili wake.
Alimwambia mama yake kwa deni alilowiwa na Adili lilikuwa kubwa sana. Hakudai lilipwe lote lakini lipunguzwe kama lilivyowezekana.
Mjeledi alimwambia Adili kuwa wema wake haukuoza. Kwa kumwokoa Huria aliwatendea wazazi wake fadhili na heshima kubwa nchi ya Majini. Ilikuwa zamu yao kumkirimu walivyoweza sasa.
Adili aliyenyamaza kwa muda mrefu alijibu, "Deni langu limekwisha lipwa lote. Niliokoa maisha ya binti yako, naye ameokoa yangu. Hapana deni tena kati yetu."
Malkia wa Majini alitabasamu akasema, "Usiseme kikembe mwanangu. Wema wako ulikuwa asilia, nawe ulitangulia kuutenda; wa binti yangu ulikuwa wa kuigiza, naye ameutenda nyuma. Asili na uigaji ni vitu mbalimbali. Havilinganiki wala havitalinganika milele."
ITAENDELEA
Featured Post
SOMA SIMULIZI ZENYE KUSISIMUA HAPA A. UTAJIRI WENYE UCHUNGU UTAJIRI WENYE UCHUNGU-1 UTAJIRI WENYE UCHUNGU-2 UTAJIRI WENYE UCH...




